Tarehe 15 Aprili, 2026, Mheshimiwa Kanali Mstaafu Kembo Dugish Campbell Muleya Mohadi, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe, amekutana kwa mazungumzo na Mheshimiwa CP-Suzan S. Kaganda, Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini humo.
Mazungumzo hayo yaliyofanyika kwenye Ofisi Ndogo za Makamu wa Rais Dkt.
Mohadi ni muendelezo wa jitihada za kimkakati kuimarisha ushirikiano wa uwili na kidiplomasia kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Zimbabwe.
Katika mazungumzo hayo, Mheshimiwa Mohadi amemshukuru Mheshimiwa Balozi Kaganda kwa kuendelea kuwa kiungo muhimu katika ya Tanzania na Zimbabwe kupitia Ofisi ya Ubalozi huku akiongeza kuwa, ushirikiano huu unaendelea kuimarika kila siku kutokana na shughuli zinazofanywa ikiwempo ziara za viongozi wa juu kutembeleana.
Aidha, Mheshimiwa Mohadi emeendelea kusisitiza kuhusu umuhimu wa kufanyika kwa Mkutano wa Tisa (09) wa JPC kati ya Tanzania na Zimbabwe kwa ajili kupitia na kupata hatua zilizofikiwa kwenye utekelezaji wa makubaliano ya Mkutano wa Nane (08). Pia, Mheshimiwa Mohadi ametoa rai ya kukuza mahusiano haya hasa kwenye eneo la Uchumi akibainisha, takwimu za uwiano wa Uchumi zilizopo haziridhishi na hivyo kunahitajika jitihada za makusudi ili kukuza uhusiano huo akitolea mfano suala la reli ya TAZARA inayoishia Zambia inaweza kusaidia katika usafirishaji wa bidhaa mbalimbali ikiwemo za nafaka kutoka nchini Tanzania.
Mheshimiwa Mheshimiwa Mohadi pia amegusia suala la ujenzi/uendelezaji wa Kituo cha Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika mradi unaotekelezwa nchini Zimbabwe ambapo inaelezwa kuwa, kukamilika kwa ujenzi huo kutasaidia upatikanaji wa taarifa, nyaraka na mabaki mbalimbali yatakayotumika kwa vizazi vijavyo katika kujifunza historia za baadhi ya Mataifa ya Afrika.
Kwa upande wake, Mheshimiwa Balozi Kaganda amemshukuru Mheshimiwa Mohadi kwa kutenga muda wake ili kujadili masuala mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Zimbabwe, ushirikiano ambao ni wa muda mrefu. Aidha, Mheshimiwa Balozi Kaganda amemjulisha Mheshimiwa Mohadi kuhusu utayari wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufanya Mkutano wa Tisa (09) wa JPC kati ya nchi hizi mbili na kwamba kinachosubiriwa kwa sasa ni mapendekezo ya tarehe za kufanyika kwa mkutano huo.
Aidha, Mheshimiwa Balozi Kaganda aliongeza kuwa, Ubalozi unatoa madarasa ya Lugha ya Kiswahili kwa hapa Zimbabwe na kwamba kwa upande Zimbabwe asilimia kubwa ya wanaofanya mafunzo ni kutoka Idara za Uhamiaji na vyombo vya ulinzi na usalama kwa ujumla.


